Hali ya upatikanaji maji kwa matumizi ya binadamu mkoani Mwanza siyo nzuri, ikichangiwa na uharibifu mkubwa wa mazingira. Hata hivyo, pamoja na hali hiyo, vyanzo vya kuaminika vya maji katika mkoa huu vinajumuisha: Ziwa Victoria, rasilimali ya maji ardhini (Visima virefu, vya kati, vifupi na vya asili), Mito, Mabwawa ya maji ya kujengwa, chemichemi na uvunaji wa maji ya mvua kwa paa za nyumba.
Miradi ya aina mbalimbali ya maji safi na salama inaendelezwa katika wilaya zetu. Chanzo cha maji cha Ziwa Victoria ambacho ni cha kuaminika bado hakijatumika ipasavyo hata katika kumpatia maji mwananchi anayeishi kando kando ya ziwa hili. Hali ya usafi wa maji katika ziwa hili siyo nzuri na, kwa kweli chanzo hiki bado hakijanufaisha ipasavyo wakazi wa mkoa huu katika kuwapatia maji safi na salama. Katika mkoa, kuna miradi ya maji ya bomba ipatayo 40 kutoka kwenye chanzo cha Ziwa Victoria na mingi ya miradi hiyo haifanyi kazi kutokana na sababu mbalimbali, zikiwemo ukosefu wa mitambo na pengine na uhaba wa madawa ya kusafishia maji hayo na hususan ukosefu wa fedha.
 |